Idara ya Habari-MAELEZO
Idara ya Habari-MAELEZO

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Idara ya Habari-MAELEZO

  • Mwanzo
  • Kuhusu Sisi
    • Idara ya Habari
    • Dhima na Dira
  • Utawala
    • Watumishi wa Idara
    • Muundo wa Idara
    • Vitengo
  • Huduma zetu
    • Ukumbi wa Mikutano
    • Taratibu za leseni
    • Kitambulisho cha Mwanahabari
    • Tozo za Huduma
  • Machapisho
    • Sheria
    • Kanuni
    • Fomu
    • Majarida
  • Kituo cha Habari
    • Taarifa kwa Umma
    • Video
    • Hotuba
    • Picha za Mnato
  • Miradi
    • Miradi iliyokamilika
    • Miradi Inayoanza
    • Miradi Ijayo
  • Dawati la Matangazo

Rais Dkt. Magufuli Azindua Hifadhi ya Taifa ya Burigi-Chato

Posted on: July 9th, 2019

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 09 Julai, 2019 amezindua Hifadhi ya Taifa ya Burigi-Chato iliyoundwa baada ya kuunganishwa kwa Mapori ya Akiba ya Burigi, Biharamulo na Kimisi yaliyopo katika Wilaya za Biharamulo, Ngara, Karagwe na Muleba Mkoani Kagera na Chato Mkoani Geita.

Hifadhi hiyo inakuwa ni ya 3 kwa ukubwa hapa nchini ikiwa na jumla ya kilometa za mraba 4,702, ikitanguliwa na Hifadhi ya Taifa ya Ruaha (kilometa za mraba 20,300) na Serengeti (kilometa za mraba 14,763).

Sherehe za uzinduzi wa hifadhi hiyo zimefanyika katika Kijiji cha Katete, Wilaya ya Chato Mkoani Geita na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwemo Mawaziri na Naibu Mawaziri, Makatibu Wakuu, Mabalozi wanaoziwakilisha nchi mbalimbali hapa nchini, Viongozi Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama, Wakuu wa Mikoa na Wilaya, Viongozi wa Dini, Viongozi wa vyama vya siasa na viongozi wa taasisi zilizo chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii.

Kabla ya kuzindua hifadhi hiyo Mhe. Rais Magufuli amekagua gwaride la Jeshi Usu la Wanyamapori na Misitu, ameshuhudia Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Hamis Kigwangallah akiwavalisha vyeo Makamishna wa Uhifadhi wa Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA), Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA), Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) na Wakala wa Misitu Tanzania (TFS), amepokea tuzo ya Hifadhi ya Serengeti iliyopata ushindi wa kuwa hifadhi bora Barani Afrika kwa mwaka 2019 na tuzo ya Mlima Kilimanjaro ulioshinda kwa kuwa kivutio bora Barani Afrika kwa mwaka 2017 na pia amekabidhi vyeti kwa wawekezaji 6 waliotayari kuwekeza katika Hifadhi ya Taifa ya Burigi-Chato.

Kabla ya hotuba yake, Mhe. Rais Magufuli aliwataka wote walioshiriki uzinduzi wa hifadhi hiyo kusimama kwa dakika 1 kwa ajili ya kuwakumbuka watu 7 wakiwemo wafanyakazi 5 wa kituo cha Televisheni cha Azam TV waliopoteza Maisha katika ajali ya barabarani iliyotokea jana asubuhi kati ya Igunga (Tabora) na Shelui (Singida) baada ya basi walilokuwa wakisafiria kuja kurusha matangazo ya uzinduzi huo kugongana uso kwa uso la lori la mizigo.

Katika hotuba yake, Mhe. Rais Magufuli ameipongeza Wizara ya Maliasili na Utalii na wadau mbalimbali kwa juhudi kubwa zilizofanyika katika uhifadhi wa maliasili ikiwemo hifadhi za wanyamapori hali iliyowezesha uoto wa asili kurejea na idadi ya Wanyama kuongezeka, wakiwemo Tembo ambao wameongezeka kutoka 43,330 mwaka 2014 hadi zaidi ya 60,000 na Faru ambao wameongezeka kutoka 15 hadi kufikia 167 hivi sasa.

Mhe. Rais Magufuli amesema kuanzishwa kwa Hifadhi ya Taifa ya Burigi- Chato kulikotanguliwa na kutangazwa kwa Pori la Akiba la Ibanda kuwa Hifadhi ya Taifa ya Ibanda-Kyerwa na Pori la Akiba la Rumanyika-Orugundu kuwa Hifadhi ya Taifa ya Rumanyika-Karagwe ni juhudi za Serikali ya Awamu ya Tano za kuendeleza sekta ya uhifadhi na utalii ambapo sasa Tanzania inakuwa na eneo la hifadhi lenye jumla ya kilometa za mraba 361,594 sawa na asilimia 32 ya eneo la nchi nzima na hivyo kuwa nchi yenye eneo kubwa lililohifadhiwa kuzizidi hata nchi ambazo ni kubwa zaidi ya Tanzania kwa eneo Barani Afrika.

Mhe. Rais Magufuli amesema pamoja na juhudi mbalimbali zilizofanywa kuhifadhi maliasili hapa nchini zikiwemo kuanzishwa hifadhi mpya, kutekeleza mkakati wa kuendeleza utalii katika Kanda ya Kusini kwa gharama ya shilingi Bilioni 340 na kuongeza mapambano dhidi ya ujangili, Serikali imechukua hatua nyingine madhubuti za kukuza utalii na uhifadhi zikiwemo kujenga na kuboresha viwanja vya ndege 11 hapa nchini, kununua ndege 8 ambapo 6 zimeshawasili na kuanza kutoa huduma za usafiri wa anga na kutekeleza mradi mkubwa wa katika mto Rufiji ambao utazalisha megawati 2,115 za umeme zitakazosaidia kupunguza matumizi makubwa ya kuni na mkaa ambao husababisha ekari 400,000 za miti kukatwa kila mwaka.

Ameongeza kuwa hatua hizo zimeanza kuzaa matunda kwani idadi ya watalii wanaotembelea hapa nchini imeanza kuongezeka kutoka watalii 1,100,000 mwaka 2015 hadi kufikia watalii 1,500,000 mwaka 2018 na kwamba yapo matumaini makubwa ya kufikia malengo ya watalii 2,000,000 mwaka 2020.

Mhe. Rais Magufuli ameitaka Wizara ya Maliasili na Utalii kuongeza juhudi za kuwavutia watalii zaidi zikiwemo kupunguza gharama za utalii, kuboresha hoteli za watalii, kupanua vivutio na huduma kwa watalii na kuwa na watoa huduma za utalii wazuri.

Aidha, Mhe. Rais Magufuli ameitaka Wizara ya Maliasili na Utalii kuwapa motisha wote wanaofanya kazi nzuri za uhifadhi na kukuza utalii hapa nchini, na katika hilo amemtaka Waziri Dkt. Kigwangallah kuwapa zawadi viongozi walioshiriki katika operesheni ya kuwaondoa wavamizi na wafugaji waliokuwa wameingiza mifugo katika Pori la Akiba la Burigi wakiongozwa na aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Kagera Meja Jen. Mstaafu Salum Kijuu ambaye amezawadiwa shilingi Milioni 10 na Cheti, Wakuu wa Wilaya Shilingi Milioni 5 na Cheti kila mmoja na viongozi wengine waliopatiwa shilingi Milioni 2 na Cheti.

“Mimi nafahamu jinsi Meja Jen. Mstaafu Kijuu alivyofanya kazi kubwa ya kusafisha pori hili lilipovamiwa na wafugaji, nilimpa siku 3 awe ameondoa mifugo yote na kweli ndani ya siku 3 mifugo iliondoka na matokeo yake leo tuweza kuanzisha Hifadhi ya Taifa hapa, kabla yake ilikuwa haiwezekani, nakupongeza sana Meja Jen. Mstaafu Kijuu, Wakuu wa Wilaya na wote walioshiriki katika operesheni ile” amesema Mhe. Rais Magufuli.

Kuhusu zawadi ya sanamu ya Baba wa Taifa aliyopewa na Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kutambua mchango wake wa kuyaenzi maono ya Baba wa Taifa, Hayati Mwl. Julius Kambarage Nyerere, Mhe. Rais Magufuli ameshukuru kwa zawadi hiyo na ameagiza wizara ijenge jengo litakalohifadhi sanamu hiyo ndani ya hifadhi ya Burigi- Chato na jengo hilo liitwe Kambi ya Kijuu (Kijuu Camp). 

Mhe. Rais Magufuli ametoa wito kwa Mabalozi na wawekezaji mbalimbali wa ndani na nje ya nchi kujitokeza kuwekeza katika maeneo ya hifadhi ambayo kwa sasa yana fursa nyingi na pia ametoa wito kwa Watanzania kuhakikisha wananufaika na kuinuka kwa utalii hapa nchini.

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamis Kigwangallah amesema kuanzishwa kwa Hifadhi ya Taifa ya Burigi-Chato kunafanya idadi ya Hifadhi za Taifa kuongezeka kutoka 16 hadi 19 na kwamba wizara hiyo inaendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuboresha huduma kwa watalii ikiwemo kujenga hoteli 3 za nyota 3 katika maeneo ya hifadhi, hosteli, kujenga gati za maboti ya watalii, barabara na viwanja vya michezo katika hifadhi.



Gerson Msigwa

Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU

Chato

09 Julai, 2019

Matangazo

  • Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari May 03, 2023
  • Baraza la Mawaziri April 14, 2023
  • Uzinduzi wa ‘The Royal Tour’ katika Ukumbi wa Guggenheim uliopo Manhattan, Jijini New York nchini Marekani April 19, 2022
  • Launch of 2019 SADC Media Awards February 13, 2019
  • Angalia zote

Habari Mpya

  • Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akisaini nakala 3 za Sheria za Tanzania zilizofanyiwa urekebu kwa mujibu wa kifungu cha 17 cha Sheria ya urekebu wa sheria, Ikulu Chamwino Mkoani Dodoma tarehe 23 Aprili, 2025.

    April 23, 2025
  • The Global Goalkeepers Award

    February 04, 2025
  • Mkutano wa Tatu wa Nchi zinazozalisha Kahawa Barani Afrika

    January 28, 2025
  • Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Masuala Nishati

    January 28, 2025
  • Angalia zote

Wasiliana Nasi

Makole, Uhindini

S.L.P: S.L.P 677, Dodoma

Simu: +255-22-2771005

Nukushi:

Email: maelezo@mawasiliano.go.tz

Simu ya Kiganjani:

Kiunganishi cha Haraka

  • Fomu ya Kitambulisho cha Mwanahabari
  • Kanuni za Sheria za Huduma za Habari za Mwaka 2017
  • Sheria ya Huduma za Habari ya Mwaka 2016
  • Fomu ya Kitambulisho cha Mwanahabari aliyopo nje ya Tanzania
  • Maelezo Podcasts (Apple Podcasts)
  • Maelezo Podcasts (Spotify)
  • Maelezo Podcasts (Amazon Music)
  • Tanzania 'THE ROYAL TOUR'
  • Tanzania 'The Royal Tour' AMAZON
  • HOTUBA YA WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI MHESHIMIWA NAPE MOSES NNAUYE (MB.), AKIWASILISHA BUNGENI MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA FEDHA KWA MWAKA WA FEDHA 2022/23
  • Baraza la Mawaziri
  • RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHE. SAMIA SULUHU HASSAN AKIHUTUBIA KATIKA MKUTANO WA 76 WA BARAZA KUU LA UMOJA WA MATAIFA (UN) TAREHE 23 SEPTEMBA, 2021 JIJINI NEW YORK, NCHINI MAREKANI
  • NCHI YETU - MIAKA 61 YA UHURU
  • NCHI YETU - Miaka Miwili na Samia
  • Mjadala maalum kuhusu mpango wa uwekezaji katika Bandari zetu!

Viunganishi Linganifu

  • Tovuti Kuu ya Serikali
  • Tovuti ya Utumishi
  • Tovuti ya Ofisi ya Rais Zanzibar
  • Tovuti ya Ofisi ya Waziri Mkuu
  • Tovuti ya Ofisi ya Makamu wa Rais
  • Tovuti ya Rais-IKULU
  • Southern African Development Community
  • Tovuti ya Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Video za Hivi Karibuni

More Videos
    • Sera ya Faragha
    • Kanusho
    • Ramani

Hakimiliki ©2023 Habari - MAELEZO